
Ninawezaje Kukua katika Hekima?
3 September 2026Je, Mariamu Alizaliwa Bila Dhambi?
Maswali magumu huhitaji majibu magumu. “Je, Mariamu alizaliwa bila dhambi?” si swali gumu; na jibu ni rahisi na moja kwa moja: La. Basi. Biblia inasema wazi: “Hakuna mwenye haki hata mmoja” (Warumi 3:10). Mariamu si tofauti. Kisha Paulo hoji kwamba “Kwa hiyo, kama kwa mtu mmoja dhambi iliingia ulimwenguni, na kwa dhambi hiyo mauti; na hivyo mauti ikawafikia watu wote, kwa sababu wote wamefanya dhambi.” (Warumi 5:12).
Kama ingekuwa kwa Biblia peke yake, makala haya yangekuwa yameisha. Lakini kwa kuwa Kanisa Katoliki halitambui Maandiko kama mamlaka ya mwisho kabisa, linatoa jibu tofauti kabisa.
Kila tarehe 8 Desemba, Sherehe ya Bikira Maria Mkingiwa Dhambi ya Asili huadhimishwa. Wakati huu, Kanisa Katoliki hutafakari imani kwamba Maria mwenyewe alihifadhiwa kutokana na dhambi ya asili. Mtazamo huu umekuwa sehemu ya mafundisho na ibada za Kikatoliki kwa karne nyingi, lakini ni hadi mwaka 1854 ndipo imani ya mkingwa dhambi ya asili ilipotangazwa rasmi na Papa Pius wa Tisa kuwa dogma—imani ya lazima na isiyoweza kubadilishwa—ya Kanisa Katoliki la Kiroma. Haya ndiyo maneno halisi ya dogma hiyo katika waraka wa kipapa Ineffabilis Deus:
Tunatangaza, kutamka, na kufafanua kwamba lile fundisho linalosema kuwa Bikira Maria Aliyebarikiwa, tangu wakati wa kwanza kabisa wa kutungwa kwake mimba, kwa neema na upendeleo wa kipekee wa Mungu Mwenyezi, na kwa kuzingatia stahili za Yesu Kristo, Mwokozi wa wanadamu, alihifadhiwa asiguswe na doa lolote la dhambi ya asili, ni fundisho lililofunuliwa na Mungu, na kwa sababu hiyo, lazima lishikiliwe kwa uthabiti na kwa kudumu na waamini wote.
Licha ya lugha thabiti na ya mwisho ya kutangaza, kufafanua, na kudai, ni vigumu kukubaliana na dogma hii ya Kimariamu kwa mtazamo wa kibiblia. Hakuna hata dalili ndogo ya ushahidi wa imani hii katika Biblia. Je, maoni ya aina hii yanawezaje kupandishwa hadi hadhi ya dogma iwapo Neno la Mungu,hasa, limenyamaza juu yake?
Daima inavutia kusikiliza jinsi theolojia ya Kikatoliki inavyotetea fundisho la kutungwa mimba kwa Maria bila doa kwa kujaribu kuliunganisha na mafundisho ya Maandiko. Tukio moja muhimu katika muktadha huu ni hotuba iliyotolewa na Papa Francisko tarehe 8 Desemba 2016. Katika hotuba yake, Papa alidai kwamba Yesu hakuja akiwa mtu mzima “aliyekua na mwenye nguvu,” bali aliamua “kufuata safari ya mwanadamu” kama Yule “aliyefanywa sawa na sisi katika kila jambo, isipokuwa jambo moja… dhambi.” Kwa sababu hiyo, “alimchagua Maria, kiumbe pekee asiye na dhambi, asiye na doa.” Alibainisha kwamba malaika anapomrejelea Maria, “anaitwa ‘aliyejaa neema,’ jambo ambalo Papa alilichukulia kumaanisha kwamba tangu mwanzo “hakukuwa na nafasi kwa dhambi” ndani yake. Kisha akasema, “Na tunapomgeukia yeye, nasi hutambua uzuri huu: humwomba, ‘aliyejaa neema,’ bila kivuli cha uovu.”
Rejeo la kibiblia alilolitaja Papa ni Luka 1:28, ambako Maria anaitwa na malaika Gabrieli kama “aliyepewa kibali.” Vuligata, tafsiri ya Kilatini ya Biblia ya mwishoni mwa karne ya nne, hutafsiri kauli hii kama “gratia plena” (“aliyejaa neema”), jambo lililofungua mianya ya dhana potofu mbalimbali, kana kwamba Maria alikuwa na ukamilifu wa neema ndani yake. Tafsiri hii imechukuliwa kumaanisha kwamba alikuwa amejaa neema kiasi kwamba lazima awe alitungwa mimba bila dhambi ya asili.
Hata hivyo, hakuna dalili yoyote katika Maandiko inayoonyesha kwamba Mariamu “amejaa” neema na hivyo “asiye na dhambi.” Kuwa “amepata kibali” humaanisha kwamba yeye, kama sisi sote, ni mpokeaji asiyestahili wa neema ya Mungu. Hili linatiwa nguvu zaidi na ukweli kwamba Mariamu anamwita Mungu “Mwokozi wake” (Luka 1:47), jambo linaloonyesha kwamba anajiona mwenye kuhitaji wokovu wa Mungu, sawa na wanadamu wengine wote. Hakuna neema ya kiasili ndani yake inayokuwapo pasipo kibali cha Mungu na uwepo wake pamoja naye.
Hivyo basi, inaonekana kwamba hoja ya utungaji mimba usio na doa wa Maria inategemea tafsiri yenye dosari ya kifungu hicho, na hivyo kusababisha fundisho lisilo na mashiko linaloathiri anthropolojia na soteriolojia, na kuvuruga mafundisho ya msingi ya Injili ya Kibiblia. Mafundisho ya wazi ya Maandiko ni kwamba “kwa sababu wote wamefanya dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu” (Rum 3:23). Hakuna marejeo yoyote kuhusu utoaji maalum kwa mtu yeyote. Mariamu hakuokolewa kwa “kuhifadhiwa” kutoka na dhambi. Alikuwa mwenye dhambi kama mwanadamu yeyote, na dhambi yake ilifanyiwa upatanisho na Mwana kwa sababu alikuwa sehemu ya ubinadamu ulioanguka uliorithi dhambi ya Adamu. Yesu ni Adamu mpya, aliyezaliwa pasipo dhambi, ili kuwaokoa wazao wa Adamu wenye dhambi, akiwemo Mariamu.
Ukweli kwamba Kanisa Katoliki la Roma limejifunga kikamilifu na fundisho la utungwa mimba usio na doa wa Mariamu bado linawakilisha alama kubwa ya kuuliza kwa wale wote wanaotaka kuisimika imani yao juu ya yale yanayofundishwa na Biblia. Ukatoliki, unaoonyesha kwa namna ya kipekee kupitia Mariolojia yake iliyosukwa kwa ustadi, haujajengwa juu ya Maandiko peke yake bali uko kwenye mkondo ambamo ibada na mapokeo yanaweza kuwa na neno la mwisho juu ya—na kinyume na—Biblia.
Makala haya yalichapishwa awali kwenye Blogu ya Ligonier Ministries.


