Jinsi ya Kusoma Manabii
17 February 2026
Jinsi ya Kusoma Simulizi ya Kihistoria
24 February 2026
Jinsi ya Kusoma Manabii
17 February 2026
Jinsi ya Kusoma Simulizi ya Kihistoria
24 February 2026

Jinsi ya Kukumbuka na Kutenda Biblia

Kujifunza Biblia ni kama kujifunza lugha. Njia bora ya kujifunza zote mbili ni kwa kuzama ndani yake. Watoto wetu wanapojifunza kuzungumza, kusoma, na kuandika, wanajifunza Kiingereza kwa kurudia, kufanya mazoezi, na kutumia. Kwa hiyo, tunaposoma Neno la Mungu, baadhi ya njia bora za kukumbuka Maandiko ni kwa kuyasoma mara kwa mara, kuyaomba mioyoni mwetu, kuyashirikisha katika maisha ya familia, na kuyasikia yakihubiriwa. Kwa maneno mengine, kadri tunavyojumuisha Maandiko katika maisha ya kila siku na kuyatumia, ndivyo tutakavyokumbuka na kuthamini yaliyomo.

1. Kusoma Biblia yote mara kwa mara.

Kwanza, tunapaswa kuisoma Biblia nzima mara kwa mara. Vitu vya kwanza tunavyohitaji katika kujifunza lugha ni msamiati, sarufi, na yaliyomo. Cha kufurahisha, Zaburi 1 haishauri waumini kutafakari sheria ya Mungu mchana na usiku; inachukulia kwamba tunafanya hivyo (Zab. 1:2). Hata hivyo, waumini wengi hawajui jinsi ya kutafakari juu Maandiko. Waanzie wapi? Hatua ya kwanza iliyo wazi ni kuisoma.

Inaonekana Wakristo wengi hawaisomi Biblia nzima. Tukitathmini ni kiasi gani tulichosoma, je, tunagundua kuwa tunavutiwa na maandiko tunayopenda kama vile Injili au Warumi 8? Hata hivyo, tunapaswa kuthamini kila sehemu ya Neno la Mungu, ikiwa si kwa sababu nyingine yoyote, ila ni kwa sababu ni Neno la Mungu. Zaburi 119 ilionyesha upendo wa dhati kwa sheria ya Bwana kwa sababu mwandishi wa zaburi alilenga upendo wa dhati kwa Bwana wa sheria. Tunahitaji eneo zima la Maandiko ili kupata picha kamili ya jinsi Mungu alivyo na Yeye ni nani. Njia bora ya kufanya hivi ni kuwa na mpango.

Ingawa mipango mingi ya kusoma ipo, kusoma sura tatu hadi nne kwa siku kutakuwezesha kupitia Biblia yote kwa takriban mwaka mmoja. Kadri tunavyosoma kila sehemu ya Maandiko mara kwa mara, ndivyo sehemu hizo zinavyoeleza kila moja, tunapoanza kuchambua msamiati wa kibiblia, sarufi, na mitindo ya mawazo. Ikiwa hatutengi muda kwa ajili ya ibada ya binafsi ya kila siku, tukipitia kwa utulivu Kitabu cha Mungu, basi tutawezaje, kama Apolo, kuwa “hodari katika Maandiko” (Matendo 18:24, KJV)?

2. Kuomba kupitia usomaji wetu wa Biblia.

Kusoma Maandiko hakupaswi kuwa tu ni maonyesho ya “ibada” ya binafsi. Ni tendo la ibada ambalo kwalo tunamtafuta Mungu, ambalo tunalieleza hasa kupitia maombi. Hatupaswi tu kuomba kwamba Mungu afungue macho yetu kuyaona mambo ya ajabu kutoka kwa sheria Yake (Zab. 119:18), lakini pia tunapaswa kuingiza maelezo ya maandiko katika maombi yetu. Kuuliza, “Andiko hili linanionyesha nini kumhusu Mungu?” kunaweza kufanya vifungu rahisi na vigumu kuwa na matunda.

Kwa mfano, Zaburi 90:1–2 inasema kwamba Mungu ni makao yetu katika vizazi vyote, na kwamba “tangu milele hadi milele” Yeye ni Mungu. Je, hatuwezi kuomba, “Bwana, nakushukuru kwamba mimi na watoto wangu tunakaa na Wewe na Wewe na sisi, na kwamba kwa sababu Wewe ni wa milele, unaweza kutimiza ahadi Zako kwa familia yetu milele”? Kutafuta utukufu wa Mungu kupitia maombi kunaweza pia kutuvuta kwa Mungu katika ibada, hata kupitia sura tisa za ukoo katika kitabu cha kwanza cha Mambo ya Nyakati, kwa kuwa tutaona uaminifu wa agano la Mungu kwa watu Wake badala ya orodha tu ya majina.

3. Kuunganisha Maandiko katika ratiba zetu za familia.

Tunajua kwamba kumpenda Bwana kunahusisha kuzungumza Neno Lake kwa watoto wetu tunapoketi, tunapoinuka, na tunapotembea (Kumb. 6:6–7). Njia iliyo wazi zaidi ya kufanya hivi ni kupanua ibada zetu za binafsi kuwa ibada ya familia, kusoma, kuomba, na kuimba kupitia Maandiko pamoja. Kufanya ibada ya familia kuwa fupi na rahisi kunafanya nyakati hizi kuwa na faida na bora kuliko kutofanya kabisa.

Kusoma na kuomba kupitia Biblia peke yetu, na katika nyumba zetu, kunatupelekea kwa urahisi kuzungumza kuhusu Biblia siku nzima. Wanandoa wanapozama katika Neno la Mungu, wakijumuisha watoto ikiwa wanao, wanajenga tabia za ibada zinazowasaidia kujua na kukumbuka Maandiko, ambayo huingia kwa urahisi katika mazungumzo ya kila siku. Kadiri tunavyoweka Maandiko moyoni, ndivyo kinywa kitakavyosema kama mafuriko ya moyo.

4. Kusikia mahubiri ya kibiblia mara kwa mara.

Katika mahubiri ya uaminifu juu ya Biblia, tunasikia sauti ya Kristo (Rum. 10:14–17; Efe. 2:17). Nguvu ya Roho inafuatana na wahubiri wanaotangaza ushuhuda wa Mungu kwa Mwanawe (1 Kor. 2:1–5). Ingawa kusikiliza mihadhara na mahubiri ya Biblia mitandaoni ni vizuri, kukutana na Kristo na watu wake katika ibada ya umma ni bora zaidi. Kwa bahati nzuri, Bwana ametupa Sabato ya kila wiki ili kuelekeza mioyo yetu kuelekea mbinguni, ambako Kristo aliyefufuka na kupaa yuko. Ibada ya faragha na ya kifamilia husaidia kutuzamisha katika Maandiko katika maisha yote. Hata hivyo, ibada ya umma ni kilele cha mchakato huu, ambapo Roho hasa huleta Neno mioyoni, akituwezesha kutenda Neno la Mungu na kulikumbuka kwa kulitenda.

Kama vile Augustine alivyoshauri katika kitabu chake On Christian Doctrine (Mafundisho ya Kikristo), njia bora ya kusoma Biblia ni kumtafuta na kumfurahia Mungu kuipitia hiyo. Maneno kwenye ukurasa ni “alama” zinazoelekeza kwa Bwana, lakini Mungu wa Utatu ni “kitu” ambacho tukinataka kweli tunaposoma na kusikia Neno la Mungu. Kujifunza Maandiko ni ushirikiano wa nafsi nzima. Je, tunaomba Roho amtukuze Mwana tunapojifunza Neno Lake? Je, tunalenga kumtukuza Mungu kwa mwili na roho kama watoto wake wapendwa? Je, tunatafuta kuikumbuka Biblia kwa kutumia njia za kuipokea yote na kwa kuiombea iweze kutekelezwa?

Makala hii ni sehemu ya mkusanyiko wa Hemenitiki (taaluma ya ufasiri wa Biblia).

Ryan McGraw
Ryan McGraw
Dr. Ryan M. McGraw ni Morton H. Smith Profesa wa Theolojia ya Kimsingi katik Greenville Presbyterian Theological Seminary na ni mhudumu katika Kanisa la Orthodox Presbyterian. Yeye ni mwandishi wa vitabu kadhaa, ikiwa ni pamoja na The Day of Worship, The Ark of Safety na A Divine Tapestry.