
Kusudi la Mungu Msalabani lilikuwa ni nini?
20 June 2025
Sababu Inayotumika katika Kuhesabiwa haki.
23 June 2025Msimamo wa uhuru wa maamuzi ya uzazi: unamaanisha Nini?
Je, ni nini kiini cha uhuru wa maamuzi ya uzazi? Ikiwa mwanamke anasema kwamba yeye binafsi asingetoa mimba lakini hataki kumnyima haki mtu mwingine kufanya hivyo, ni kwa misingi gani mwanamke huyu angesita kutoa mimba? Labda anataka tu kuwa na watoto wengi iwezekanavyo na haoni kama atakumbana na ujauzito usiotakikana. Labda mtu huyu hufikiri kwamba kijusi ni binadamu hai au hana uhakika kuhusu hali ya kijusi. Pengine anaamini kwamba kijusi ni binadamu aliye hai lakini hataki kulazimisha mtazamo huu kwa wengine. Hapa tunafikia kiini cha msimamo wa uhuru wa maamuzi ya uzazi. Je, haki ya kuchagua ni haki isiyo na masharti wala mipaka? Je, tuna haki ya kimaadili kuchagua kile ambacho ni kibaya kimaadili? Kuuliza swali kama hilo ni kulijibu.
Tena, kila sheria iliyopitishwa inapunguza au kuzuia uchaguzi wa mtu. Hiyo ndiyo asili halisi ya sheria. Ikiwa hatutaki kuzuia chaguo la watu wengine kupitia sheria, lazima tuache kutunga sheria na kuacha kupiga kura. Nadhani kwamba watu wengi watakubali kwamba uhuru wa kuchagua si uhuru usio na masharti wala mipaka. Hakuna mwanadamu yeyote aliye sheria kamili kwa nafsi yake. Isipokuwa tuko tayari kukubali mfumo wa Imani ambao unashikilia kwamba maarifa na maadili ni mambo ya mpito yanayotawaliwa na uwezo wa ubongo na wakati, basi sheria na jamii zinakuwa haziwezekani, lazima tukimbie kama upepo kutoka kwenye dhana kwamba mtu binafsi yupo huru kabisa. Ili kuhama kutoka kwenye dhana kuelekea kwenye hali halisi, nashangaa kama wanaharakati wanaounga mkono uhuru wa maamuzi ya uzazi wanapinga sheria zinazolinda haki zao za mali ya kibinafsi? Je, mwizi anayevunja nyumba ili kuiba televisheni ya mtu ana haki isiyoweza kuondolewa ya kufanya uamuzi huo? Je, mwanamume ana haki ya kuchagua kumbaka mwanamke? Mifano hii ya kupindukia inaonyesha wazi kwamba uhuru wa kuchagua hauwezi kuchukuliwa kama haki isiyo na masharti wala mipaka.
Je, uhuru wa kuchagua unapaswa kumalizikia wapi? Ninaamini unamalizikia pale ambapo uhuru wangu wa kuchagua unakanyaga haki za msingi za mtu mwingine za maisha na uhuru. Hakuna mtoto ambaye hajazaliwa ambaye amewahi kuwa na haki ya kuchagua au kukataa uharibifu wake mwenyewe. Kwa kweli, kama wengine walivyosema, mahali pa hatari zaidi nchini Marekani kwa mwanadamu ni ndani ya tumbo la uzazi la mwanamke. Kwa mamilioni ya watoto ambao hawajazaliwa, tumbo la uzazi limekuwa kama seli ya hukumu ya kifo. Mfungwa anauawa mara moja bila faida ya kesi au neno la utetezi. Utekelezaji huu unahusisha kukatwa kiungo hadi kiungo. Je, maelezo haya ni bayana sana? Je, ni ya kuchochea hisia kupita kiasi? Hapana. Ingekuwa tu ikiwa maelezo haya hayakuwa ya kweli.
Haki ya kuchagua, ingawa inaweza kuwa takatifu, haibebi haki ya kiholela ya kuharibu maisha ya binadamu. Huku ni sawa na kuavya haki kama ilivyo kuavya mtoto wa binadamu.
Ni nini kuhusu uhuru wa kuchagua kinachoufanya kuwa wa thamani sana? Nini kilichomchochea Patrick Henry kusema, “Nipe uhuru au nipe kifo”? Kwa hakika tunatamani kuwa na uhuru wa kujitawala, na wazo la kuishi chini ya msukumo wa nje linachukiza. Sisi ni viumbe tunaofikiri, na tunathamini uhuru wetu wa kufanya maamuzi. Wengi wetu tungechukia kufungwa, lakini hata katika gereza lenye ulinzi mkali, haki ya mtu ya kuchagua haiondolewi kabisa.
Ni hii kanuni ya kujitawala—kuwa na nafasi ya kusema kuhusu hali yangu na mustakabali wangu—ndiyo inayonyimwa kikatili kila mtoto ambaye hajazaliwa, mimba iliyotolewa. Sikuwa na kauli katika uamuzi wa mama yangu kama atafanya utoaji mimba au kunizaa. Maisha yangu yote yalikuwa mikononi mwake. Kama angechagua kutoa mimba, maisha yangu yangekuwa yamezimwa kabla sijazaliwa. Wewe na mimi tu binadamu halisi. Wakati mmoja tulikuwa hatuwezi kutumia haki yetu ya thamani ya kuchagua. Wakati mmoja tulikuwa tunategemea kabisa chaguo la mtu mwingine kwa ajili ya uwepo wetu wenyewe.
Kipengele cha pili muhimu cha haki ya kuchagua ni swali la lini kufanya uamuzi wa kimaadili kuhusu maisha ya mtoto. (Kwa sababu hii inahusisha maadili ya kijinsia, ni hoja isiyopendwa sana katika mjadala.) Wakati wa kuchagua kuwa na mtoto au la si baada ya mtoto kutungwa na kuanza kukua. Isipokuwa katika kisa cha ubakaji, kujamiiana kwa kutumia au bila kutumia mpango wa uzazi bado ni suala la uchaguzi. Chaguo tunalofanya, iwe la asili ya kujamiana au lisilo la asili ya kujamiana, daima huwa na matokeo. Ni kanuni ya maadili na sheria kwamba tunawajibika kwa matokeo ya chaguo letu.
Wakati tunapojamiana, huenda hatuna nia au hamu ya kuzalisha maisha ya mwanadamu mwingine. Tunafahamu, hata hivyo, kwamba kujamiiana huanzisha mchakato wa uzazi na kunaweza kuzalisha mtoto. Kuua kijusi siyo njia ya kuwajibika au ya kimaadili ya kushughulikia uamuzi huu.
Dondoo lililochukuliwa kutoka utoaji wa mimba na R.C. Sproul.
Makala haya yalichapishwa kwanza katika Blogu ya Huduma za Ligonier.


